Quantcast
Channel: ziro99blog
Viewing all articles
Browse latest Browse all 4529

ACHINJWA KIKATILI MBELE YA MKWE WAKE MPANDA

$
0
0
Mkazi wa Kijiji cha Mwamkulu wilayani Mpanda, Suzana Kingi (40), ameuawa kikatili  na watu wasiofahamika kwa kuchinjwa akiwa katika chumba alicholala, huku mkwe wake akishuhudia.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari, alisema jana kuwa mauaji hao  ya kinyama, yanahusisha imani za kishirikina na yalitokea juzi usiku wa manane nyumbani kwa  marehemu katika Kijiji cha Mwamkulu.
Kidavashari  alisema usiku  huo  wa tukio, Suzana alikuwa amelala peke  yake nyumbani kwake, jirani na nyumba  walimolala wake wa mwanawe, Paul Charles, ambao ni  Maria  Kanyungiro na Maria Nsabi. 
Ilidaiwa kuwa wakati mke wa kwanza, Maria Kayungiro akiwa  chumbani kwake, alisikia  mama mkwe akikimbia kutoka  nyumbani kwake akienda  kwenye nyumba walimokuwa wamelala wakweze, huku akipiga mayowe  ya kuomba  msaada akisema  ‘mama  nakufa ....nakufa... nisaidieni.’
Mama mkwe wake  alipofika  katika nyumba walimolala wakweze, alisukuma kwa nguvu mlango  wa chumba alichokuwa amelala mke wa pili, Maria Nsabi na kuingia chumbani  huku akihema  kwa hofu na akiendelea kupiga mayowe.
Kamanda Kidavashari alidai kuwa  watu hao,  ambao  hawakufahamika mara moja  wakiwa  na silaha za jadi  yakiwemo  mapanga, walikuwa wakimfuata kwa nyuma  wakimfukuza.
Inadaiwa wauaji waliingia ndani  ya chumba hicho, wakitumia mwanga  wa kurunzi na kumkuta Suzana amejilaza na mke huyo wa pili wa mwanawe kitandani.
Kwa mujibu wa madai ya Kamanda Kidavashari, wauaji hao  walianza kumshambulia  Suzana  kwa mapanga  na  hatimaye  kumchinja.
Mke wa pili wa mwanawe, Nsabi, alishuhudia  unyama  huo  kimya kimya,  kwa madai kuwa alionywa asipige kelele  na kwamba kama angejaribu, angeuawa kama mama  mkwe  wake, Suzana.
 “Ilipotimu  saa kumi  alfajiri, Paul  alirejea  nyumbani  kwake akitokea  harusini  katika  kijiji  cha jirani na  alipoingia  chumbani  kwake,   alimkuta  mkewe Maria Nsabi  akiwa  amezirai  sakafuni.
“Akiwa hajajua cha kufanya akajikuta amekaa kitandani ghafla  akamwona mama yake mzazi  akiwa  ametapakaa  damu  mwili  mzima tayari  ameaga dunia,“ alieleza Kamanda Kidavashari.
Uchunguzi wa awali  wa  mkasa huo, kwa mujibu wa Kamanda Kidavashari,  unaonesha kuwa  chanzo  za mauaji  hayo ni imani  za kishirikina na mpaka sasa  hakuna mtu yeyote  aliyekamatwa kuhusishwa na tukio hilo.
Kidavashari amewaasa  wananchi  kutoa ushirikiano  kwa Jeshi  la Polisi ili  kuweza kuwabaini  wahalifu  hao  ili  sheria  iweze kuchukua  mkondo wake.

Viewing all articles
Browse latest Browse all 4529

Trending Articles