Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imefuta ushahidi wa aliyekuwa Kamishna wa Kodi wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Felesian Msigala, uliokuwa umetolewa mahakamani hapo kwa ajili ya kumtetea aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba.
Jopo la majaji watatu linalosikiliza kesi hiyo, lilitoa uamuzi huo jana baada ya kukubali ombi la Wakili wa Mramba, Peter Swai aliyeomba Mahakama kumuondoa shahidi huyo pamoja na ushahidi alioutoa.
Mramba na wenzake wanakabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia Serikali harasa ya Sh bilioni 11.7.
Akiwasilisha ombi hilo, Wakili Swai aliiomba Mahakama kumuondoa shahidi huyo pamoja na ushahidi alioutoa mahakamani hapo ili waendelee na mashahidi wengine wanaomtetea Mramba.
Aidha aliomba kesi hiyo iahirishwe kwa kuwa mashahidi waliotakiwa kufika Mahakamani wanashughulikia mambo ya kitaifa, upande wa Jamhuri ulidai hauna pingamizi na kuomba kesi itakaposikilizwa upande wa utetezi walete shahidi zaidi ya mmoja.
Msigala alitoa ushahidi huo kwa ajili ya kuunga mkono utetezi wa Mramba hata hivyo upande wa Jamhuri ulipinga kwa madai kuwa hastahili kuwa shahidi katika kesi hiyo kwasababu ushahidi alioanza kuutoa unaonesha amefika mahakamani hapo kama mtaalamu wa masuala ya kodi na siyo shahidi wa kumtetea Mramba.
Jopo la majaji wanaosikiliza kesi hiyo, Jaji John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela lilikubali kufuta ushahidi huo katika kumbukumbu za Mahakama na kuahirisha kesi hiyo hadi Julai 17 na Agosti 15 itakapotajwa na itasikilizwa Agosti 21 mwaka huu.
Mbali na Mramba, washitakiwa wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo ni Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu wa zamani wa Wizara ya Mipango na Uchumi, Gray Mgonja.
Katika utetezi wao Mramba atakuwa na mashahidi wanne na Yona mashahidi watatu.
Washitakiwa wanadaiwa kati ya Agosti mwaka 2002 na Juni 14, 2004 jijini Dar es Salaam, wakiwa watumishi wa umma, walitumia vibaya madaraka yao na kuisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 11.7 baada ya kutoa msamaha wa kodi kinyume cha sheria kwa Kampuni ya M/S Alex Stewart ya nchini Uingereza.