![]() |
Jaji Frederick Werema. |
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alisema hayo juzi katika semina maalumu ya wajumbe hao kuhusu Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Jaji Werema alisema katika mijadala ya Bunge Maalumu, kila mjumbe atakuwa na uhuru huo wa maoni, ambao umeainishwa katika Sheria hiyo kifungu 27(2).
Alisema wajumbe hao hawakuwekewa mipaka ya kujadili Rasimu ya Katiba isipokuwa kwa kiwango kinachotajwa, huku akisisitiza kutogusa misingi mikuu ya Taifa na maadili ya kijamii.
"Wabunge wa Bunge Maalumu la Katiba wawe huru na wavulimiane, waheshimu uhuru wa afya ya mawazo katika eneo hili, ili tujenge mwafaka wa kitaifa katika masuala yenye maslahi kwa Taifa," alisema Jaji Werema.
Alisema kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Bunge hilo limepewa jukumu maalumu la kihistoria la kuandaa Katiba mpya.
"Huu ni Mkutano wa Taifa wa Maridhiano. Lugha zetu ziwe ni za maridhiano ya maana," alisema Jaji Werema na kuongeza:
"Kutokana na hayo yote, ni vema kila mjumbe wa Bunge Maalumu akatambua na kutimiza wajibu wake kwa mujibu wa sheria."
Aidha, katika kufanikisha suala hilo, kila Mjumbe anapaswa kuzingatia kuisoma kwa makini Rasimu ya Katiba ili kubaini maudhui ya masharti ya Rasimu hiyo.
Mengine ni kushiriki kwenye mchakato wa kutunga Kanuni za Bunge Maalumu ambazo ni msingi na dira ya shughuli zote za Bunge hilo; kushiriki kikamilifu katika vikao, mijadala au shughuli zote za Kamati za Bunge Maalumu.
Kushiriki kikamilifu katika mijadala ya pamoja ya Bunge Maalumu na kuleta mawazo chanya ili kufanikisha upatikanaji wa Katiba inayopendekezwa.
Kuweka maslahi ya Taifa mbele ya maslahi mengine yoyote, ili kudumisha umoja wa kitaifa na mwafaka wa pamoja katika kufikia malengo yaliyokusudiwa katika Bunge Maalumu la Katiba.
"Kujenga na kudumisha haiba ya kuvumiliana wakati wa mijadala katika kamati za Bunge Maalumu na vikao vya Bunge Maalumu kwa ujumla," alieleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Bunge Maalumu la Katiba lenye wajumbe 629 linatarajiwa kuanza rasmi mijadala wiki ijayo baada ya kupitishwa kwa kanuni zake, ambazo ndizo zitasimamia mwongozo wa majadiliano hayo baada ya kukabidhiwa Rasimu ya Katiba.