![]() |
Baadhi ya majeruhi wa mlipuko huo wa bomu wakipatiwa matibabu hospitalini. |
Mtu asiyefahamika aliyerusha bomu kwa mkono katika mkutano wa kampeni za uchaguzi wa madiwani wa Chadema katika kata ya Soweto mkoani Arusha, imebainika aliandaliwa mazingira ya kutoroka ili asikamatwe na mkono wa sheria.
Akitoa kauli ya Serikali bungeni jana kuhusu tukio hilo la kigaidi lililotokea katika mkutano wa siasa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi, alisema polisi walizuiwa kumfikia mhalifu.
"Mkutano huu ulikuwa na ulinzi wa Polisi wakiwa na magari mawili na askari walisimama upande wa Kaskazini ya uwanja na mrushaji wa mlipuko huo alikuwa upande wa Mashariki ya uwanja huo na akarusha kuelekea Magharibi.
"Jaribio la Polisi kutaka kumfuata aliyerusha mlipuko huo, zilizuiwa na makundi ya wananchi ambao walianza kushambulia polisi kwa mawe na kuwazomea na hivyo polisi wakalazimika kujiokoa badala ya kumsaka mhalifu," alisema Lukuvi kwa masikitiko.
Lukuvi alitaka kila Mtanzania ajihoji kwa nini wananchi walishambulia na kuzuia askari kutimiza wajibu wao, badala ya kusaidia wamkamate mhalifu.
Lukuvi alikumbusha kwamba pamoja na umuhimu wa Polisi katika maisha ya kila Mtanzania, lakini siku za karibuni, kumekuwa na jitihada za makusudi za baadhi ya vyama vya siasa, makundi ya kijamii na watu binafsi kupandikiza chuki kwa raia dhidi ya vijana wa Polisi.
Juhudi hizo kwa mujibu wa Lukuvi, zimesababisha raia wachukie askari, wasiwaamini, wasitoe ushirikiano ili hatimaye lengo la kuhakikisha Taifa halitawaliki, litimie.
"Askari hawa ni ambao wanajitolea usiku na mchana, ili Watanzania wenzao wawe salama. Hawa ni askari ambao wanauawa kila siku na majambazi wakiwa wanatutetea, hawa ni askari ambao ni watoto wa Taifa hili nao ni Watanzania wanaofanya kazi za hatari kwa ajili yetu," alikumbusha.
Lukuvi alitaka wananchi wakumbuke kuwa Polisi ina wajibu wa kisheria na kikatiba kulinda watu na mali zao na wanapokuwa kwenye mikutano ya hadhara, ya kijamii au ya kisiasa, wanakuwa pale ili kulinda raia na wanaaga familia zao kuwa wanakwenda kazini kulinda raia.
Shambulio hilo la bomu ni la pili katika matukio ya kuvunja amani na sehemu ya mfululizo wa matukio ya kuvuruga amani nchini ambapo Lukuvi alisema aina ya urushaji wa bomu hilo, hautofautiani na mbinu iliyotumika katika shambulio la Mei 5, katika Kanisa Katoliki Parokia ya Olasiti mkoani humo.
"Shambulio la Soweto limehama kutoka kanisani sasa ni katika mikutano ya kisiasa. Nia ni ile ile ya kufanya Watanzania wachukiane, wapigane na Taifa letu liparaganyike," alisema.
Alituhumu baadhi ya wanasiasa kushiriki mpango wa kuparaganyisha Taifa, au kuhakikisha nchi haitawaliki, lakini kwa kujua au kutojua wanaendelea kutoa kauli za chuki.
"Wanadhani wanajiimarisha kisiasa, kumbe wanapanda mbegu ya uharibifu wa Taifa letu, itakayozaa chuki, vita na majuto makubwa," alisema Lukuvi.
Pamoja na jitihada zilizokwishafanywa za kumtafuta mtuhumiwa, ikiwemo ya Polisi kupata taarifa ya mwonekano wa mtu aliyerusha bomu hilo, Lukuvi alisema Serikali inatangaza dau la Sh milioni 100, kwa watakaotoa taarifa za kumpata mhalifu huyo.
Alifafanua, kwamba kila atakayetoa taarifa atapata Sh milioni 10 na hata wakiongezeka Serikali itaongeza fedha hizo. Aliwahakikisha wenye taarifa hizo kuwa, watapewa ulinzi na taarifa zao zitakuwa za siri.
Lukuvi pia alitaka Watanzania wa dini zote, makabila yote na vyama vyote, waungane kukabiliana na adui wa sasa ambaye alisema ni mbaya kuliko Nduli Idi Amini, aliyeshambulia Kagera ambaye Watanzania waliungana kukabiliana naye na kumshinda.
"Adui wa sasa ni mbaya zaidi kwa kuwa anataka kutupiganisha wenyewe kwa wenyewe, aivunje nchi kwa mikono yetuÉtuwakemee na kuwakabili maadui hawa, wawe wa ndani au nje na tuape kuilinda na kuitetea nchi yetu. Tuape kuendeleza upendo, umoja na mshikamano wa Watanzania," alisema.
Kutokana na hali hiyo Spika wa Bunge, Anne Makinda, jana aliitisha kikao cha Kamati ya Uongozi ya Bunge, ili kujadili na kutoa kauli ya Bunge kuhusu bomu hilo.
Mbali na kuitisha kikao hicho, pia aliruhusu mjadala bajeti ya Serikali ianze kwa wabunge kutoa maoni yao bila kuwapo Bajeti kivuli ya Kambi Rasmi ya Upinzani kutokana na uamuzi wa Chadema kuondoa wabunge wake wote bungeni na kuwapeleka Arusha bila taarifa rasmi kwa Spika.
Kabla ya kuruhusu mjadala wa bajeti kuanza, Mbunge wa Chakechake, Musa Haji Kombo (CUF), aliomba Mwongozo wa Spika akiitaka Serikali kuacha kutoa taarifa ya bomu hilo la Arusha, badala yake itoe taarifa ya matukio yote ya kuvunja amani ya kuanzia Zanzibar mpaka Arusha.
Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR-Mageuzi), aliomba Bunge liahirishe shughuli zake, wajadili tukio hilo na kuongeza kuwa amepitia katika mitandao ya kijamii na kukuta wafuasi wa CCM na Chadema wakitupiana mpira.
Machali alipendekeza ikiwezekana vyama hivyo viwili vifutwe na Msajili kwa kuwa Tanzania ni zaidi ya CCM na Chadema.
Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi), aliporuhusiwa kuomba Mwongozo, alitaka viongozi wazee wasiwaachie vijana mzigo wa nchi isiyo na amani wakati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliwaachia nchi yenye amani.
Alitaka Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utawala Bora, George Mkuchika anayeshughulikia Usalama wa Taifa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi, wajiuzulu kwa alichosema ni kushindwa kukamata wahalifu.
Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), aliitaka Serikali itenganishe tukio hilo na siasa na kuongeza kuwa inaonekana inamjua mtuhumiwa na kuhoji kama inamfahamu, kwa nini iunde kikosi cha uchunguzi.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo, Abdallah Alila (40) ameeleza namna alivyoona mtuhumiwa wa kurusha bomu lililoua watu watatu na kujeruhi 68, akikimbizwa na watu waliokuwa kwenye mkutano wa Chadema.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Alila ambaye ni mkazi wa Arusha, alidai kuwa alikuwa pembeni mwa gari la matangazo katika mkutano huo, kwenye viwanja vya Soweto.
"Wakati viongozi wa Chadema wakimaliza kunadi wagombea niliona kitu kama mfuko wa nailoni (Rambo) ukirushwa juu na ulipotua kulitokea mlipuko mkubwa ambao ulitikisa eneo zima," alisema.
Aliendelea kusema: "Mimi nilianguka kwenye mtaro nikiwa nimeumia miguuni, nilipoinuka niliona watu wakimkimbiza mtu anayedaiwa kuwa mhusika aliyerusha mfuko ule wa plastiki uliosababisha mlipuko.
"Nilisikia kelele za watu wakimkimbiza mtu anayedhaniwa kurusha mfuko huo, lakini kila walipojaribu kumkamata walishindwa na wengine kuanguka".
Alisema mtu huyo ambaye ni mwanamume, alikimbilia karibu na hospitali ya Kaloleni huku sauti kutoka kwa baadhi ya watu zikisema, "Yule! Yule!"
Mmoja wa wakazi wa eneo hilo la Soweto katika nyumba za AICC, ambaye hakutaka jina lake liandikwe, alisema baada ya mlipuko, kulikuwa na heka heka ikiwamo watu kukimbia hali iliyomlazimu kukimbilia ndani kuokoa maisha ya wanawe.
Serikali ya Marekani imelaani tukio hilo ikisema: "Tunatoa pole kwa familia za waliopoteza maisha na waliojeruhiwa katika uhalifu huo uliopindukia. Tukio hili la uoga limetokea baada ya lingine la Mei 5 katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi mkoani humo, ambapo watu watatu waliuawa na zaidi ya 60 kujeruhiwa.
"Tunatoa mwito kukamatwa, kushitakiwa na kuhukumiwa kwa wahusika," amesema Balozi wa Marekani nchini, Alfonso Lenhardt.
Katika taarifa yake jana, Balozi alisema Tanzania inajulikana kuwa nchi inayothamini tofauti za kitamaduni na kuvumiliana; na kwamba vitendo vya uhalifu kama hivi, bila kujali vinafanywa na nani vinatishia kuchafua na kudhalilisha amani na usalama wa nchi hii tukufu.
Alisema msimamo wa Marekani ni kudumisha ushirikiano na Watanzania wote na kuwataka waendelee kukataa matukio kama haya yanayofanywa na wanaotaka kuhatarisha maisha ya wananchi wenzao.
"Tunawataka wananchi wote kuenzi kwa uangalifu mkubwa amali za busara, umoja, na amani zilizoanzishwa na Baba wa Taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere, ambazo zimekuwa siku zote zikitamkwa hata katika Wimbo wa Taifa.
"Ni amali ambazo zimekuwa zikienziwa na Watanzania wote na wapenda amani wenzao duniani kote," alisema Balozi Lenhardt katika taarifa hiyo.
Makamu wa Rais Dk Mohamed Gharib Bilal amesema Serikali itafanya kila linalowezekana kuhakikisha inabaini kiini cha milipuko inayotokea mara kwa mara jijini Arusha kwani inafanya wakazi kushindwa kufanya kazi za uzalishaji mali.
Dk Bilal alisema hayo jana alipotembelea majeruhi zaidi ya 63 wa mlipuko huo. "Tunataka kujua kiini cha milipuko na ikiwezekana kuidhibiti kabisa kwani inafanya wakazi wa Arusha kushindwa kufanya kazi," alisema.
Alitembelea majeruhi walioko hospitali za Mount Meru, Selian na Elizabeth ambapo aliwapa pole na kusema Serikali inaungana na wafiwa katika kuomboleza.
Wakati Makamu wa Rais akimaliza, Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana nao waliwasili Arusha kwa lengo hilo.
Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Selian, Dk Paul Kisanga alieleza kuwa watoto wawili ndugu Fatma na Farida Jumanne wamepelekwa hospitali ya Aga Khan jijini Nairobi, Kenya kwa matibabu zaidi.
Mtoto mwingine Amir Ally (7) alifariki dunia na kufanya idadi ya marehemu kuwa watatu ambao ni Judith Moshi (25) ambaye ni Katibu wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) kata ya Sokon One, Arusha na Ramadhan Juma (15) ambao wote walikufa kutokana na mlipuko huo.
"Madaktari wetu na wauguzi walijitahidi kuokoa maisha ya mtoto Amir lakini bahati mbaya hawakufanikiwa kutokana na madhara aliyopata kichwani na hivyo kupoteza maisha," alisema Dk Kisanga.
Daktari huyo aliongeza kuwa kuhusu mtoto Fahad Jamal (7) ambaye yuko Chumba cha Wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) wanasubiri kuwasili kwa timu ya madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kutokana na hali yake kutoruhusu kusafirishwa kwenda hospitali nyingine.
"Timu hiyo ya madaktari bingwa watafanya tathmini, hali yake na kama kuna uwezekano watampeleka nje ya nchi kwa matibabu zaidi pamoja na wagonjwa wengine ambao bado wanaendelea na matibabu," aliongeza.
Alisema kwa sasa idadi ya majeruhi waliobaki hospitalini hapo ni 37 na inaweza kuongezeka kutokana na ujio wa madaktari bingwa wanaotarajiwa kupokea majeruhi kutoka hospitali ya Mount Meru na St Elizabeth.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alitoa pole kwa viongozi wa Chadema na wanachama wote na akalaani kitendo hicho na kuongeza kuwa Serikali kupitia Wizara yake itatoa msaada wa ndege kupeleka majeruhi itakapohitajika.
"Pia tutatoa msaada wa dawa na vifaa vingine kwenye hospitali zote ambazo wamelazwa majeruhi wote; za Mount Meru, Selian na St.Elizabeth," aliongeza.
Wakati polisi ikiwa inaendelea na kazi ya kusaka wahusika waliofanya kitendo hicho, tukio hilo limegeuzwa la kisiasa kutokana na baadhi ya vyama vya siasa kunyoosheana vidole.
Mwenyekiti wa Chadema , Freeman Mbowe amedai Chadema wana ushahidi wa kutosha wa watu waliohusika na tukio hilo.
"Tuna ushahidi wa kutosha wa picha za video na za kawaida kuhusu waliohusika na tukio hilo la kinyama la kurusha bomu katika mkutano wetu juzi," alidai Mbowe.
Alitoa madai hayo jana nje ya Hospitali ya Selian baada ya kutembelea majeruhi pamoja na kumjulia hali Mbunge wa Arumeru Mashariki ambaye pia amelazwa hapo baada ya kushambuliwa.
Nassari ambaye alikuwa Meneja Kampeni Kata ya Makuyuni, Monduli alishambuliwa na kujeruhiwa kichwani na watu wanaodaiwa kuwa wafuasi wa CCM.
Mbowe alidai chama hicho kina ushahidi wa mikanda ya video ambayo inaonesha aina ya bomu la kutupa na mkono na kwamba aliyerusha ni askari wa kikosi cha Polisi wa Kutuliza Ghasia (FFU).
Mbowe pia alidai magari mawili ya Polisi aina ya Toyota Land Cruiser rangi ya bluu likiwa na askari wawili nyuma na gari aina ya Land Rover TDI yalitumika kufanya shambulio hilo.
Alitamba, kuwa wataanika ushahidi wote kwa umma, hivyo hata kama ukweli utafichwa, wao watatoa ukweli wa jambo hilo kwa watu pamoja na vyombo vya sheria na Umoja wa Mataifa (UN).
Alisema hivi sasa wanasheria wa chama hicho, Tundu Lissu, Profesa Abdallah Safari na Mabere Marando watatoa kauli juu ya tukio hilo.