Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jana imezindua rasmi usambazaji wa matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 kimkoa na kuanza na Mkoa wa Pwani.
Uzinduzi huo uliambatana na semina kwa watendaji wa mkoa huo, uliofanywa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mwamtumu Mahiza.
Mkoa huo umekuwa wa kwanza kusambaziwa matokeo hayo, ili waangalie takwimu za mkoa huo zilivyo na kuzitumia kupanga miradi ya maendeleo kwa wananchi.
Mahiza (pichani) alisema NBS wameanza kusambaza matokeo ya sensa hiyo kwenye mkoa huo kwa wakati, kwani hivi sasa wanajiandaa kupanga bajeti ya mkoa kwa mwaka ujao wa fedha.
Alisema matumizi ya takwimu halisi na bora ni jambo la msingi ambalo linapaswa kufuatwa na watendaji kuanzia ngazi ya kijiji, ili kupanga miradi ya maendeleo kwa makini kwa kuzingatia mahitaji ya maeneo husika.
"Tuwashukuru NBS, wameanza hapa kwetu kusambaza matokeo ya sensa na hili limekuja kwa wakati, tupo kwenye kuandaa bajeti ya mkoa wetu hivyo tutatumia matokeo ya sensa hiyo kupanga bajeti yetu,"alisema Mahiza.
Aidha alisema ni vyema watendaji kwenye ngazi mbalimbali kuanzia mkoa hadi kijiji wakawafafanulia wananchi kwenye maeneo yao juu ya matokeo hayo, ili waangalie jinsi ya kupanga miradi ya maendeleo kulingana na mahitaji ya eneo husika.