Jopo la marais wa zamani wanaoshughulikia mgogoro wa Ziwa Nyasa baina ya Tanzania na Malawi, linasaubiri kumalizika kwa uchaguzi Mkuu wa Malawi unaotarajia kufanyika Jumanne ijayo, ili kuingia katika awamu ya pili ya mazungumzo ya kumaliza mgogoro huo.
Hayo yalisemwa juzi na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimatifa, Bernard Membe, kufuatia swali la mwandishi mmoja wa Malawi aliyetaka kujua msimamo wa sasa wa Tanzania kuhusu mgogoro huo.
Waziri Membe alikuwa jijini Blantyre, Malawi, akiongoza ujumbe wa Tanzania uliosafirisha mwili wa aliyekuwa balozi wa nchi hiyo nchini Tanzania, Flossie Gomile-Chidyaonga, aliyefariki ghafla jijiji Dar es Salaam ijumaa iliopita. Mwili huo ulisafirishwa kwa ndege ya serikali ilyotolewa na Rais Jakaya Kikwete, jambo ambalo limewakuna wananchi wa Malawi wakiipongeza hatua hiyo.
"Kama wote mnavyojua, Tanzania na Malawi zilimua kupeleka suala hili kwenye jopo linaloongozwa na Rais wa zamani wa Msumbiji, Joachim Chisano, akisaidiwa na Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki na Rais wa Mstaafu wa Botswa, Festus Mogae.
"Tulichukua uamuzi huu kutokana na uhusiano mzuri wa kindugu ambao nchi zetu, Tanzania na Malawi, tunao, kwamba badala ya kubishana sisi wenyewe kwa wenyewe tukipe chombo kingine kutazama mgogoro wenyewe na kutoa uamuzi," alisema.
Alisema kwa kuwa Malawi inafanya uchaguzi wake mkuu, jopo la marais hawa wa zamani liliona lisubiri uchaguzi huo kumalizika. Alisema baada uchaguzi, serikali itakayoingia madarakani, iwe ya sasa inayoongozwa na Rais Joyce Banda ama ya sura nyingine, basi suala hilo litazungumzwa tena katika awamu ya pili.
"Ni matumaini yetu kwamba jopo la wazee wetu hawa kwa kushirikiana na wanasheria waliobobea, watatupeleka sehemu ambayo tutajua namna nzuri ya kulimaliza suala hili na tuna imani kwamba sisi kama ndugu ambao tumekuwa tukilitumia ziwa hili karne kwa karne suala hili litapata ufumbuzi mzuri," alisema.
Alisema kwa sasa mtazamo wa Tanzania umejikita kwenye maana ya "mpaka baina ya nchi na nchi unaotokana na ziwa (mto ama bahari)."
"Hata mki-google (mkitumia injini ya google ya kutafutia habari kwenye mtandao) mtaona kwamba uamuzi wa mpaka wa Tanzania na Malawi katika eneo hili bado haujawahi kufikiwa. Kwa vile hayajawahi kuwepo mazungumzo ya kujadili mpaka uweje, kinachotakiwa, kwa mantiki hiyo, ni nchi hizi kuunda tume za mpaka kwa pamoja, kuangalia na kisha kukubaliana ni wapi mpaka kwenye ziwa hili uwe, kama ni katikati ama vinginevyo katika namna ambayo inakubaliwa kimataifa," alisema.
Mgogoro wa ziwa Nyasa ambao hata hivyo ulikuzwa sana na vyombo vya habari kuliko hali halisi, ulikuja baada ya Malawi kudai kwamba ziwa hilo lote liko nchini Malawi na kwamba mpaka ni ufukweni kwa upande wa Tanzania.
Dai hili lilileta mtazamo kwamba kwa upande wa Tanzania, mpaka ni pale yanapoanzia maji ya Ziwa Nyasa na hivyo Mtanzania anapovua samaki ama kuteka maji kwenye ziwa hilo, anakuwa ameingia nchi nyingine ya Malawi.