Meneja Mauzo wa Kampuni ya Tanzanite One, inayojishughulisha na uchimbaji, ununuzi na uuzaji wa madini ya Tanzanite nje ya nchi, amefukuzwa nchini.
Mkuu wa Uhamiaji Mkoa wa Arusha, Daniel Namomba alisema kuwa meneja huyo, Jacques Beytel (39) raia wa Afrika ya Kusini, alifukuzwa nchini (PI) Juni 13 mwaka huu.
Namomba alisema hayo jana mbele ya waandishi wa habari. Alisema kuwa Beytel alikamatwa Juni 10 mwaka huu katika ofisi za Tanzanite One baada ya kibali chake cha kufanya kazi nchini kwisha Juni 5 mwaka huu.
Mbali ya kufukuzwa nchini kwa meneja huyo, pia Kampuni ya Tanzanite One imepewa onyo kali na Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Arusha kwa kosa la kuajiri mfanyakazi bila ya kuwa na kibali wakati ikijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.
Namomba alisema kuwa mtuhumiwa huyo raia wa Afrika Kusini alifukuzwa na kusindikizwa Juni 14 mwaka huu na maofisa wa Uhamiaji kupitia njia ya Namanga hadi nchini Kenya.
Alipoulizwa ni kwa nini hawakuhakikisha wanamsafirisha hadi nchini kwao, Namomba alisema lengo lao ni kuhakikisha anatoka nchini na sio kujua anakoelekea.
Hata hivyo, kuna utata mkubwa wa kusafirishwa kwa Beytel kwani habari za uhakika zinasema kuwa mtuhumiwa huyo alisafirishwa kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa (KIA) na mmoja wa wafanyakazi wa Kampuni ya Tanzanite One kwa kutumia gari la ofisi hiyo.